Masomo ya Jumapili kwa kifupi: Maajilio 3 B
Isaya 61:1-2.10-11; Zaburi-Luka 1; 1 Wathesalonike 5:15-24; Yohana 1:6-8.19-28
Furaha ya Kweli

Wapendwa, leo ni Jumapili ya tatu ya Maajilio na nada yetu “Furaha.” Leo tunawasha mshumaa wa tatu wa rangi ya waridi kwenye taji la majilio, ishara ya furaha kwa sababu Krismasi inakaribia. Mtume Paulo katika barua yake ya kwanza kwa Wathesalonike anatualika kuwa na furaha katika Bwana kila wakati. Hata hivyo, swali ni, je, tunajua kweli furaha ni nini? Watu wa Israeli walifurahi waliposikia kwamba mwokomkombozi atakuja kwa sababu walikuwa wamepitia mateso mengi mikononi mwa wakoloni. Nabii Isaya anamtambulisha Kristo kama yule atakayewaletea habari njema watu waliokuwa wakiteseka. Mfano maskini ambaye amekuwa akisumbuka kortini kwa miaka mingi akitafuta haki ya kurejesha kiwanja chake kilichochukuliwa na mwekezaji binafsi. Ni furaha gani kwa mtu huyu wakati hukumu inapotolewa kumrejeshea kiwanja chake. Ni furaha kubwa kila wakati kupata kilichopotea. Katika Injili ya Luka 15, Yesu anatoa mifano mitatu ya hitimisho la furaha baada ya kilichopotea hatimaye kupatikana, yaani kondoo aliyepotea, sarafu iliyopotea, na mwana aliyepotea.
Furaha inaweza kufafanuliwa kama hali ya ustawi anayopitia mtu. Ni hali ya kheri. Katika Injili Mathayo 5:3-12, Yesu anataja aina tisa za watu ambao watafikia furaha. Anaanza “Heri…”. Je, unajihisi mwenye furaha maishani mwako sasa hivi?
Katika Wimbo wa Katikati leo, tunamuona Maria akifurahi juu ya ujumbe wake Malaika Gabriel. Habari Njema ya kuzaliwa kwa mwokozi. Anaimba wimbo maarufu wa magnigicat. Sisi pia tunafurahi kwa sababu mwokozi atazaliwa upya mioyoni mwetu. Hata hivyo, tunahitaji kujibu swali; je, tunaelewa kweli furaha ni nini? Je, habari ya kuja kwa mwokozi inaniletea furaha ya kweli?
Tukiangalia tabia yetu na ile ya wengine wanaotuzunguka, tunaweza kusema kwa ujumla kwamba kila mtu anatafuta furaha. Watu wanatafuta furaha sehemu nyingi na kwa njia mbalimbali. Wengine wanahisi kwamba wakiwa matajiri, au wakipata nyadhifa kubwa na ushawishi watapata furaha. Wengine bado, wanahisi kwamba furaha yao inatokana na kufanya mambo Fulani ambayo siwezi kuyataja hapa. Lakini wengine wana hakika kwamba furaha yao inatokana na kutumikia Mungu na binadamu. Ni nini kinachokupa furaha ya kweli?
Hata hivyo, furaha imethibitisha kuwa jambo lenye kuteleza sana kwa maskini na matajiri pia. Utajiri, nguvu, na vitu vya dunia havijaweza kumpatia mtu yeyote furaha ya kweli. Familia zingine zina mali yote wanayoweza kutamani Pamoja na kushikilia nafasi za nguvu, lakini hawajawahi kuonja furaha ya kweli. Wazazi wanagombana, au wameachana Watoto wamesambaratika, hawasali au kula pamoja, hawapati usingizi kwa hofu ya kushambuliwa, n.k. Familia nyingine ni maskini wanaogombana kila usiku na mchana kwa sababu wanalaumiana kwa umaskini wao. Hakuna anayeonekana kupata suluhisho kwa sababu hawafanyi kazi. Wanageukia uchawi au kutumia muda mwingi kutoka kwa nabii mmoja hadi mwingine, kutoka kituo kimoja cha sala hadi kingine. Lakini furaha kwao ni ndoto ya mchana. Swali, Je, familia yangu ina furaha?
Labda ni kwa sababu hatujui mahali pa kutafuta furaha ya kweli au tunapotoshwa. Furaha si kitu tunachoweza kuchukua na kuvaa kama tunavyofanya na nguo. Ni hali ya ustawi inayohisiwa ndani mwetu na inayong’aa kwenye mazingira yetu. Hatuwezi kuigiza furaha. Ikiwa tunataka kuwa na furaha, tunahitaji kuwekeza katika mambo yanayotuletea furaha. Tunahitaji kusikiliza ushauri wa Yohane Mbatizaji “nyoosheni njia ya Bwana.” Hatuwezi kuwa na njia zilizopotoka na kutarajia kuwa na furaha. Viongozi wafisadi hawawezi kutarajia kupata furaha. Watu wavivu hawatakuwa na furaha kwa sababu umaskini utajikita kwao. Ikiwa tutaendelea kupuuza amri za Mungu; furaha haitakaa karibu nasi. Lakini, ikiwa Kristo atakaa ndani yetu, tutakuwa na furaha ya kweli. Yesu anatuhubiria Ufalme wa Mungu, ambao unajulikana kwa haki, amani, na furaha moyoni.
Furaha ni jambo la kijamii ni uambukiza kama vile huzuni. Hakuna mtu anayeweza kuwa na furaha wakati wale walio karibu naye ni wenye huzuni. Ikiwa tunataka kweli kuwa na furaha, tunahitaji kuwekeza katika furaha ya wale walio karibu nasi. Kuna kauli mbiu kwa Kihispania inayosema, “Compartida la vida es mas,” ambayo inamaanisha, “Uhai ukishirikishwa, unaongezeka.”
Wapendwa, leo nawakaribisha tutafakari kuhusu dhana yetu ya furaha na mahali tunapoitafuta. Je, tunafanya uwekezaji unaofaa kwa furaha katika maisha yetu na familia zetu? Je, Krismasi ni chanzo cha furaha kwangu na familia yangu?
Jumapili yenya furaha.
Pd. Lawrence Muthee, SVD
